Home » » WADAU WAMWANGUKIA MRATIBU KOMBE LA MUUNGANO MUFINDI

WADAU WAMWANGUKIA MRATIBU KOMBE LA MUUNGANO MUFINDI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
WADAU wa michezo wamemwomba Mratibu wa Kombe la Muungano Mufindi, Daud Yassin, kufikiria zaidi uamuzi wake wa kustaafu kuandaa mashindano hayo na kuongeza muda zaidi wa kuratibu kwa lengo ya kuyaokoa yasife.
Kati ya waliomuomba Yassin kubatilisha uamuzi wake, ni Mkurugenzi wa Idara ya Maendeleo ya Michezo, Leonard Thadeo, ambaye alikuwa mgeni rasmi katika fainali ya kombe hilo iliyopigwa mwishoni mwa wiki kwenye Uwanja wa Shule ya Msingi Igowole, Mufindi mkoani Iringa na kushuhudiwa timu ya Benki ya Wananchi Mufindi (Mucoba), ikiibuka bingwa mpya baada ya kuwavua Mbaspo ya Mbeya.
Thadeo, alimtaka mratibu huyo kuongeza muda zaidi wa kuratibu mashindano hayo, huku akimwandaa mtu mwingine aweze kuyaendeleza.
Alisema ni uamuzi wa busara wa Yassin kung’atuka, lakini kabla ya kuachia madaraka hayo, hana budi kutengeneza mazingira kwa mtu ambaye atakuja kushika nafasi hiyo ili aweze kuendeleza mazuri ya Kombe la Muungano.
“Usiondoke ghafla ndugu yangu, kwanza weka mazingira safi kwa kumwandaa mtu ambaye ataweza kuyasimamia na shirikiana na wadau wa michezo wilayani hapa na kisha unaweza kufanya maamuzi yako ya kung’atuka,” alisema Thadeo.
Aliwataka waratibu wa mashindano hayo kupanua wigo kwa kushirikisha michezo mingine itakayohusisha jamii husika, kwa kuanzia ngazi ya kijiji hadi tarafa na kisha mikoa.
Thadeo, aliwashukuru wadau wote waliofanikisha mashindano ya Muungano kufana na waliyoyaunga mkono na kuwataka wafadhili zaidi kujitokeza katika kuyapa sapoti miaka inayokuja.
Mdau mwingine wa michezo, Alex Kalinga, alisema kuwa kustaafu kwa Yassin kuratibu mashindano ya Kombe la Muungano ni mshituko mkubwa katika tasnia ya michezo na kumtaka kuongeza miaka zaidi, kwa lengo la kumwandaa mtu mwingine aweze kuyasimamia kwa uadilifu na kuendeleza vipaji vya vijana.
Alisema mashindano ya Kombe la Muungano Mufindi, yameweza kuvumbua vipaji vingi katika Wilaya ya Mufindi na mikoa ya jirani, hivyo hofu kubwa ni kusimama kwa mashindano hayo na kufa kabisa kama Yassin ataamua kustaafu.
Alisema upeo mkubwa wa mratibu huyo ndiyo chachu ya mashindano hayo kuwa makubwa miongoni mwa jamii ya Watanzania.
“Itachukua muda sana kumpata mtu atakayevaa viatu vyake kwa sasa, hivyo ni jukumu la wadau kukaa na Yassin kuweza kujadili jinsi gani atamwachia mtu na ikiwezena aahirishe kustaafu kuandaa mashindano haya,” alisema Kalinga.
Mwalimu Wilson Ngongi, alisema Yassin ataacha mzigo mzito kwa jamii ya wanamichezo akiamua kweli kustaafu kuratibu mashindano hayo, ambayo yamejizolea mashabiki na kuvumbua vipaji kwa miaka zaidi ya 18.
Alisema Watanzania wengi ni watu wa kukwepa majukumu ambayo hayana maslahi, lakini kwa Yassin ameweza kuandaa mashindano hayo kwa fedha zake za mfukoni hadi yakawa makubwa na kushirikisha mikoa mingine ikiwemo Zanzibar.
“Naomba sana Yassin atusaidie kuendelea kukuza vipaji vya vijana, kwani hili hakuna mtu mwingine kwa sasa atakayeweza kuyaendeleza na mwisho wa siku mashindano haya yatakufa,” alisema Ngongi.
Kwa upande wake, Yassin alisema ameanza kuandaa mashindano ya Kombe la Muungano Mufindi akiwa kijana mdogo, lakini kwa sasa umefika wakati wa kustaafu na kuwaachia wengine kuyaendeleza.
 Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Blogs za Mikoa
Copyright © 2012. Iringa Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa