Home » » MUCOBA FC MABINGWA KOMBE LA MUUNGANO MUFINDI

MUCOBA FC MABINGWA KOMBE LA MUUNGANO MUFINDI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
FAINALI za 18 za mashindano ya Kombe la Muungano Mufindi zilimalizika juzi kwa Benki ya Wananchi Mufindi (Mucoba Fc), kunyakua taji kwa kuwafunga mabingwa watetezi Mbaspo Academy ya jijini Mbeya kwa changamoto ya penalti 7-5 katika mchezo mkali uliofanyika uwanja wa shule ya Msingi Igowole, Mafinga.
Katika mchezo huo ambao Mgeni Rasmi alikuwa Mkurugenzi wa Idara ya Maendeleo ya Michezo, Leonard Thadeo, hadi dakika 45 zinakamilika kuashiria mapumziko, hakuna nyavu iliyokuwa imetikiswa.
Kipindi cha pili, kilianza kwa timu zote kusomana, lakini walikuwa ni Mucoba walioanza kujipatia bao dakika ya 70 likifungwa na David Mhanga kabla ya kuongeza la pili dakika ya 75.
Mbaspo walikuja juu na kupata bao dakika ya 84 likifungwa na Soud Mlindwa kabla ya Thabit Juma kuchomoa dakika ya 90, ndipo changamoto ya mikwaju ya penalti alipochukua nafasi.
Penalti za Mbaspo zilifungwa na Eliah Jimmy, Mpoki Mwansansu, Masoud Yusuph, Soud Mlindwa na Boaz Patson huku Thabit Juma na Michael Masinga wakikosa.
Mucoba waliofunga ni Benjamin Mlowe, Ima Mwakajinga, Stanley Mwazangila, Elisha Mwasieni, Denis Lameck na Daud Mwanga huku aliyekosa ni Reward Abraham. Katika mikwaju hiyo, shujaa aliibuka Kipa wa Mucoba aliyepangua penalti mbili.
Bingwa wa mashindano hayo, Mucoba ilijinyakulia sh milioni 3, Kombe lenye thamani ya sh milioni 1.2 na medali za dhahabu, mshindi wa pili Mbaspo, iliondoka na kitita cha sh milioni 1.5, waamuzi bora Steven Makuka, Hashim Mgimba na Erasto Msalilwa waliojipatia sh 50,000 kila mmoja, mchezaji bora aliibuka Hussein Juma Igowole Sekondari aliyepata sh 200,000 mfungaji bora Shadrack Tamimu wa Mbeya City sh 200,000 na timu yenye nidhamu ikaibuka Mbeya City iliyojipatia sh 500,000 na kombe.
Kombe la Muungano Mufindi 2014 linaratibiwa na Daud Yassin na kudhaminiwa na Chai Bora, Asas Limited, Mucoba na PPF.
 chanzo :Tanzania Daima

0 comments:

 
Blogs za Mikoa
Copyright © 2012. Iringa Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa