Home » » NEWFOREST YAKABIDHI BWENI NA NYUMBA YA MWALIMU SHULE YA SEKONDARI LUNDAMATWE

NEWFOREST YAKABIDHI BWENI NA NYUMBA YA MWALIMU SHULE YA SEKONDARI LUNDAMATWE

MKUU wa Wilaya ya Kilolo mkoani Iringa Gerald Guninita amewataka wazazi na walezi wa wanafunzi wa shule kutowaruhusu watoto wao kufanya biashara zenye mazingira hatarishi, ili kuwaepusha na changamoto zinazowakwamisha wanafunzi kutomaliza masomo.
Guninita ameyasema hayo wakati akipokea msaada wa Bweni la Wasichana wa shule ya sekondari ya Lundamatwe,jengo liligharimu zaidi ya shilingi Milioni 76.8, msaada uliotolewa na kampuni ya Newforest inayojishughulisha na upandaji wa miti mkoani Iringa.
Aidha Guninita amesema baadhi ya wanafunzi wamekuwa wakiingia katika vishawishi kwa kutumiwa na wazazi/ walezi kufanya biashara zisizostahili ikiwa pamoja na uuzaji wa pombe katika vilabu, jambo linalosababisha hasa mabinti kuingia katika ngono na kupata mimba.
Amesema jamii inapaswa kuwalinda wanafunzi hasa mabinti ikiwa pamoja na wazazi kuhakikisha wanafunzi wanakaa katika mabweni, ili waweze kupata muda mwingi wa kujisomea, kutokana na ukweli kuwa wanafunzi wamekuwa wakipatiwa majukumu mengi wawapo nyumbani.
Mkuu huyo wa Wilaya ameahidi kuchangia mifuko 50 ya Saruji katika shule hiyo ili kuwaunga mkono juu ya ujenzi wa bweni lingine la wavulana, huku akiwahimiza wananchi kuchangia sekta ya elimu kwa kuwekeza zaidi kwa wanafunzi ambao ni viongozi wa siku zijazo.
Hata hivyo mkurugenzi mkuu wa Newforest Bw. Rob Newborn amesema atahakikisha kampuni yake inashirikiana vyema na jamiii inayouzunguka mradi kwa kutatua changamoto mbalimbali za wananchi ili kuleta tija ya uwepo wa kampuni yake.

0 comments:

 
Blogs za Mikoa
Copyright © 2012. Iringa Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa