Home » » KIWANDA CHA PARETO(PCT) WAPATA HASARA BILIONI 1.4

KIWANDA CHA PARETO(PCT) WAPATA HASARA BILIONI 1.4


Meneja wa kiwanda cha Pareto Martin Oweka kilichoko Wilayani Mufundi katika mji wa Mafinga.
========  ======  ========
KIWANDA CHA PARETO(PCT) WAPATA HASARA BILIONI 1.4

Na Denis Mlowe,Mufindi

KIWANDA cha Pareto(PCT) cha Wilayani Mufindi, mkoani Iringa kimepata hasara ya zaidi ya shilingi Bilioni 1.4 baada ya kushindwa kununua pareto kwa wakulima na kuizalisha kwa kipindi cha miezi miwili. Meneja wa kiwanda Martine Oweka alisema mpaka sasa mitambo ya kuzalishia zao hilo ilisimama kwa muda kutokana na kukosekana kwa malighafi hiyo baada ya kuwepo kwa wanunuzi wengi, ambao wamekuwa wakisafirisha nje ya nchi licha ya kuwepo kiwanda.

Alisema hasara kubwa inatokana na uwekezaji wao katika zao hilo ambapo, kwenye msimu wa kilimo walitumia Sh milioni 500, kuwanunulia wakulima miche ya pareto, elimu juu ya kilimo hicho sambamba na ujenzi wa maeneo ya kukaushia zao hilo, ili kuongeza sumu. " Mwezi Julai ilikuwa tupate tani 100 za pareto kwa wakulima lakini tuliambulia tani 20 wakati mwezi huu wa agosti kati ya tani 200 ambazo ilikuwa tukusanye, tumeambulia tani 30 tu, hii ni hasara kubwa sana kwetu hatukuwa na kibali cha kununua pareto kwa wakulima japo hiki ni kiwanda pekee Tanzania,”alisema Oweka.

Alisema kibali cha kununua zao hilo kwa wakulima ilikuwa wapatiwe mwezi juni mwishoni, lakini badala yake walipewa August 21, mwaka huu kikiwa kimechelewa kwa miezi miwili.Hata hivyo alisema hasara ya Sh Bilioni 1.4 waliyoipata kwa kushindwa kuzalisha zao hilo, inawaghalimu wakulima ambao, wengi wao wamehifadhi pareto ndani kinyume cha taratibu za zao hilo, ambalo ubora wake hutegemea ukali wa sumu.

“Mkulima akivuna Pareto halafu akahifadhi ndani kwenye unyevu kwa muda mrefu inapoteza sumu kiasi ambacho hata sisi wanunuzi inakuwa vigumu kuinunua kwani, ubora wa pareto ni kiwango cha sumu iliyopo,”alisema.Aliongeza kuwa kushindwa kununua pareto hiyo kumeisababishia hasara serikali kwa kuwa imekosa fedha za kigeni ambazo hutokana na mauzo ya nje ya zao hilo mara baada kuzalishwa kiwandani hapo. Aliwataka wakulima kutokata tamaa na badala yake waendelee kuzalisha zao hilo na kuiomba serikali kulinda soko la pareto.

Kwa upande wao wakulima, wameiomba serikali kuhakikisha kuwa zao hilo halifi na kuona namna ya kulinda viwanda vya ndani vyenye uhakika wa soko badala ya kuruhusu soko huria, wakati malighafi hiyo hata ndani ya nchi haitoshelezi mahitaji. Uwezo wa kiwanda cha Pareto cha Mafinga ni kuzalisha tani 6,000 kwa mwaka lakini badala yake, kimekuwa kikiambulia tani 2,5000 pekee.

0 comments:

 
Blogs za Mikoa
Copyright © 2012. Iringa Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa