Home » » Wanawake watakiwa kutambua haki zao

Wanawake watakiwa kutambua haki zao

WAWANAKE mkoani Iringa wametakiwa kuzitambua haki zao sambamba na sheria za utawala bora ndani ya jamii katika kukabiliana na vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia.
Mkuu wa Chuo Kikuu Kishiriki cha Ruaha (RUCO), Dk. Cephas Mgimwa, alitoa kauli hiyo jana wakati wa mafunzo juu ya haki za wanawake yaliyoandaliwa na Kitengo cha Haki za Binadamu na Utawala Bora wa chuo hicho kwa wanawake wa Halmashauri ya Manispaa ya Iringa.
Alisema mwanamke anapaswa kupewa nafasi za kutoa michango yao katika uamuzi mbalimbali ndani ya jamii, ikiwemo masuala ya ndoa, umiliki wa mali na masuala ya mirathi.
Alisema mafunzo hayo ya utawala bora yamelenga kuwajengea uwezo wanawake kufikia mifumo mbalimbali ya mahakama, ili kupata msaada wa kisheria kwa lengo la kukabiliana na changamoto mbalimbali zinazowakabili, zikiwemo kupigwa, kubakwa, kuachika na kunyimwa mirathi kutokana na baadhi ya mila potofu katika baadhi ya makabila.
Mgimwa alisema kumekuwa na unyanyasaji wa kijinsia katika jamii nyingi za Kitanzania, hasa watoto na wanawake walioko ndani ya ndoa na nje ya ndoa na kwa kukosa ufahamu wa sheria na haki za binadamu wengi wao wameshindwa kupeleka malalamiko yao sehemu husika.
Mhadhiri na Mkuu wa Kitengo cha Sheria wa chuo hicho, Dk. Mary Livera, alisema binadamu wote ni sawa na hakuna tofauti ya mwanamke na mwanaume katika kupata haki za msingi za binadamu.
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Blogs za Mikoa
Copyright © 2012. Iringa Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa