Home » » WAVUVI HARAMU WAHUJUMU MTERA

WAVUVI HARAMU WAHUJUMU MTERA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

 

UVUVI haramu umeelezwa na wananchi wa vijiji vya Mbweleli na Makatapola, Iringa Vijiji mkoani Iringa kuhatarisha uwepo wa baadhi ya samaki wanaopatikana katika bwawa la Mtera.

Samaki hao ni pamoja na Ngalala, Pelege Dungu, Ngogo na Ngobole ambao ukubwa wake ni chini ya inchi tatu.

"Umaskini ni moja ya sababu inayowafanya wavuvi wakiwemo wale wanaotoka katika vijiji hivi kujiingiza katika uvuvi haramu ili wakabiliane na changamoto za kiuchumi," alisema mkazi wa Kijiji cha Mbweleli, Jenirosa Mbunda.

Hayo yalielezwa katika mafunzo ya siku tatu yaliyofanywa kwa wananchi wa vijiji hivyo na Asasi ya Maendeleo ya Mazombe Mahenge (MMADEA) inayoshirikiana na Taasisi ya E Link Consult Ltd hivi karibuni mkoani hapa, kutoa elimu ya mabadiliko ya tabia nchi, kwamba wizi wa nyavu na ukosefu wa elimu ni sababu nyingine inayosababisha uvuvi haramu katika bwawa hilo.

Ofisa Uvuvi wa Halmashauri ya Wilaya ya Iringa, Nelson Mbawala alisema katika mafunzo hayo Sheria ya Uvuvi inaruhusu samaki wanaotakiwa kuvuliwa wawe na ukubwa wa nchi tatu na kuendelea.

"Ikitokea mvuvi akavua samaki ambaye hatakiwi kuvuliwa kwa mujibu wa sheria anatakiwa kumrudisha bwawani hata kama amekufa," alisema Mbawala.

Alisema, uvuvi wa kutumia makokoro unafanywa na wavuvi wengi katika bwawa hilo kwa sababu unaelezwa kuwanasa samaki wengi kwa muda mfupi ikilinganishwa na ule halali wa kutega.

Mbali na kuwamaliza samaki katika bwawa hilo, washiriki wa mafunzo hayo walisema aina hiyo ya uvuvi haijasaidia kuwakomboa kiuchumi kwa sababu ni lazima ifanywe na watu wengi zaidi.

"Ukiangalia hali zao wale wanaofanya uvuvi halali wa kutega wanaonekana kuwa na maisha bora zaidi kuliko wale wanaovua kwa kutumia makokoro yanayouzwa kwa bei kubwa," alisema Mbawala.

Katika kuwanusuru samaki hao na wengine wanaotakiwa kuvuliwa kihalali mmoja wa washiriki katika mafunzo hayo, Leonard Ndilwa alisema; "Zamani kulikuwa na utaratibu wa wavuvi kuruhusiwa kuvua kwa siku zisizozidi 20 kila mwezi na kuacha siku nyingine kumi kuwawezesha samaki kuzaliana na kukua."

Mshiriki mwingine Hussein Magomba alisema, Serikali imeshindwa kukabiliana na wavuvi wanaotumia makokoro na ndio maana uvuvi huo unaonasa samaki wadogo na wakubwa bado unaendelea.

Wengine wakasema hawawezi kuacha aina hiyo ya uvivu, labda serikali itakaposaidia kuwasambazia nyavu halali za uvuvi kwa bei ndogo.

Mshiriki mwingine Agripina Thomas alisema, shida kubwa ya wavuvi wa vijiji hivyo kujiingiza katika shughuli ya uvuvi haramu ni kutoshiriki katika shughuli nyingine za uzalishaji mali kama kilimo.

Mkurugenzi wa MMADEA, Raphael Mtitu alisema uvuvi haramu unatumia zana zinazoharibu mazingira na hivyo kuchangia mabadiliko ya tabia nchi.

Alisema katika kukabiliana na mabadiliko hayo wavuvi wanapaswa kufanya shughuli zingine za kiuchumi kama kilimo na ufugaji.

0 comments:

 
Blogs za Mikoa
Copyright © 2012. Iringa Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa