Home » » SERIKALI KUENDELEA KUWAWEZESHA VIJANA KIUCHUMI.

SERIKALI KUENDELEA KUWAWEZESHA VIJANA KIUCHUMI.


Na. Aron Msigwa- MAELEZO.
Wakati maadhimisho ya Wiki ya Vijana kitaifa  yakiingia siku ya tatu mkoani Iringa Serikali imewahakikishia vijana kuwa itaendelea na mkakati wake wa kuwawezesha vijana kiuchumi  kwa kuwapatia mikopo ili waweze kukabiliana na changamoto mbalimbali za kimaisha na kuondokana na umasikini.
Akizungumza na Vijana wanaoshiriki maadhimisho hayo mkoani Iringa Naibu Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo Mh. Amos Makala amesema  kuwa serikali katika kuhakikisha inatimiza lengo hilo kwa kuanzia imetenga kiasi cha shilingi bilioni 6.1 katika bajeti ya mwaka 2013/2014 ili kuwawezesha vijana kote nchini.
“Jambo hili la kuwawezesha vijana tunalipa uzito mkubwa na kwa kuanzia katika bajeti ya mwaka huu tumetenga kiasi cha shilingi bilioni 6.1 kuwawezesha vijana, ni mwanzo mzuri pamoja na kuwa tunahitaji kufanya zaidi” amesema
Amefafanua kuwa kiasi  hicho cha fedha kitatolewa kwa vijana walioamua kujishughulisha na wenye mawazo ya kujikwamua kiuchumi na kuwataka vijana kote nchini kutumia fursa ya mikopo wanayopata kuitumia katika kufanya shughuli za maendeleo.
“Nawaomba vijana muepuke kutumia fedha hizo katika anasa na mambo mengine yasiyokusudiwa yanayowafanya  mjikute  mmeingia katika matatizo ya madeni na kuendelea kuwa maskini” amefafanua
 Hata hivyo amesema  serikali kwa kuliona jambo hilo imeandaa mpango wa kuwapatia elimu vijana ili waweze kuzitumia ipasavyo fursa za maendeleo zilizopo na waweze kujiandaa kunufaika na kiasi hicho cha fedha zilizotengwa pia  inafanya jitihada za kuboresha vyuo vya  vijana pamoja na  kuongeza  idadi ya walimu wa vyuo hivyo.
“Nataka niwahakikishie kuwa serikali inaendelea kuviboresha vyuo vyetu vya ndani ikiwa ni pamoja na kushirikiana na nchi marafiki ambapo kwa kushirikiana na Afrika ya Kusini tunaandaa utaratibu wa kupeleka walimu wetu ili waweze kusoma huko na kuja kufundisha vijana katika vyuo vyetu” amesema.
Mh. Makala ameongeza kuwa tayari serikali katika kushughulikia tatizo la  ajira hasa kwa vijana wanaohitimu masomo ya elimu ya juu kwa kuzungumza na baadhi ya taasisi za fedha zikiwemo benki za NMB, EXIM Bank na CRDB ili ziweze kutoa mikopo kwa vijana hao kwa dhamana ya vyeti vyao na kubainisha kuwa tayari baadhi ya benki zimekwisha anza zoezi la kuwakopesha vijana kwa kutumia dhamana ya vyeti vyao.
Aidha kuhusu maadhimisho ya Wiki ya Vijana kitaifa amesema kuwa inatokana na uamuzi waserikali uliofanyika mwaka  1999 mjini Dodoma wa kuhakikisha kuwa kila mwaka vijana wanapata fursa ya kujumuika pamoja katika maadhimisho hayo.
Aidha amewashukuru viongozi wa mkoa wa Iringa kwa maandalizi mazuri waliyoyafanya ya kwa kushirikiana na viongozi wa Wizara ya Habari Vijana , Utamaduni na Michezo kuhakikisha kuwa shughuli za Wiki ya Vijana na kilele cha mbio za Mwenge wa Uhuru tarehe 14/10/2013 zinafanikiwa kwa kiwango kikubwa.
“Sisi kama viongozi wa Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo  tunawashukuru  sana viongozi wa Iringa kwa ushirikiano mlioutoa katika kufanikisha  shughuli hizi za Wiki ya Vijana kitaifa, na ni matumaini yetu kuwa tarehe 14 mwezi huu wananchi wengi zaidi watajitokeza katika kilele cha Mbio za Mwenge wa Uhuru 2013” amesema  Mh. Makala.
Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Maendeleo ya Vijana Bw. James Kajugusi  amesema kuwa maadhimisho ya mwaka huu yanalenga kuwafanya vijana kujitambua na kuwakumbusha kuzitumia fursa za kimaendeleo zilizo katika maeneo yao kujiletea maendeleo.
Amesema  katika maadhimisho ya mwaka huu licha ya kuwepo kwa maonyesho ya bidhaa mbalimbali zilizotengenezwa na vijana kutoka mikoa mbalimbali nchini vijana watapata fursa ya kujadili mada mbalimbali katika midahalo ikiwemo mada ya kuujua mkoa wa Iringa na fursa za kimaendeleo na ajira zilizopo katika mkoa wa Iringa, pia huduma za hifadhi ya jamiii na maendeleo ya vijana,nafasi ya vijana wa Tanzania katika kutunza amani na upimaji wa hiari wa maambukizi ya Virusi vya Ukimwi.
Naye Mkuu wa Mkoa wa Iringa Dkt. Christine Ishengoma  amesema kuwa mkoa wa Iringa utaendelea kutoa msukumo kwa vijana ili waweze kujiletea maendeleo kutokana na fursa zilizopo ndani ya mkoa huo.
Ameongeza kuwa mkoa huo kwa muda mrefu umekuwa na jukumu la  kuwaandaa vijana kuwa watu wanaojitegemea, kuwa viongozi na watoa maamuzi sahihi, wajasiriamali na wazazi wanaowajibika na kuongeza kuwa serikali ya mkoa kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wameendelea kutoa elimu kwa vijana kuhusu uzazi salama, ujasiriamali na kujikinga dhidi ya maambukizi ya Ukimwi.
Dkt. Ishengoma ameeleza kuwa mkoa wa Iringa umeanzisha mfuko wa kuwawezesha vijana kwa kuwapatia mikopo na mitaji ya kuendesha miradi midogo midogo  ya kiuchumi na kuondoa tatizo za utegemezi  na tayari vikundi vipatavyo 70 katika halimashauri za mkoa wa  Iringa katika mwaka 2012/2013 vimepatiwa kiasi cha zaidi ya shilingi milioni 116.

0 comments:

 
Powered by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Iringa Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa