Home » » Mwenge wazindua kituo cha soka Iringa

Mwenge wazindua kituo cha soka Iringa

KITUO cha kisasa cha Iringa Football for Hope Centre kilichoko chini ya Shirika la Vijana, Walemavu na Watoto (IDYDC), la mkoani hapa na kufadhiliwa na Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA), kimezinduliwa rasmi na mbio za Mwenge.
Akisoma risala kwa Kiongozi wa mbio za Mwenge, Lige Masanja, alisema kituo hicho kina lengo la kukuza vipaji vya mpira na kutoa elimu na ushauri nasaha kwa vijana.
Alisema hadi kukamilika kwake, kimegharimu sh milioni 275 zilizotokana na ufadhili wa FIFA.
Naye Kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru, Juma Ally Simai, aliishukuru FIFA kwa msaada wa kituo hicho na kuwataka vijana kutambua kuwa michezo ndiyo njia pekee ya kuwaunganisha katika kuleta amani na upendo katika jamii.
Simai alisema kupitia michezo watu wengi wameweza kuondokana na chuki, hivyo ni jukumu la kila mmoja kupenda michezo ambayo ni yenye nafasi kubwa ya kutatua tatizo la ajira.
Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa TFF, Angetile Hosia, alilipongeza Shirika la IDYDC kwa kukamilisha mradi huo na kitendo hicho kitakuza soka ya vijana kwa Mkoa wa Iringa na taifa kwa ujumla na kuwataka kutumia ipasavyo kituo hicho katika kufanikisha kukuza vipaji vya soka.
Alisema kwa kufanikisha kituo hicho, utakuwa mwanzo wa FIFA kutoa fedha zaidi kwa ajili ya miradi kama hiyo nchini na kuitaka serikali iongeze kasi katika ujenzi wa viwanja bora kwa lengo la kukuza michezo nchini.
Naye Mkurugenzi wa IDYDC, Johnnie Nkoma, alisema lengo la kituo ni kuwafikia watoto 8,000 lakini kitaanza kuwahudumia 200 kwa sasa na kuwataka watoto wajitokeze kupata nafasi ya kujifunza michezo mbalimbali.
Nkoma alisema kituo hicho kitakuwa kinatumika usiku na mchana, kwani wanafunzi na watoto watakuwa wakipata mafunzo nyakati za jioni wakati vijana na watoto wa mitaani watakitumia usiku kwa ajili ya mazoezi ya kukuza vipaji vyao.
“ Katika kituo hiki vijana watakuwa wanapata mafunzo ya afya ya uzazi na ugonjwa wa ukimwi, pia watapata nafasi ya kujua afya zao kwa kupima ukimwi bure hapa hapa kituoni, kutoa ujuzi wa mpira wa miguu na kutoa elimu ya kuimarisha uwezo wa vijana kuondokana na matumizi ya madawa,” alisema Nkoma.
Alizitaja huduma zitakazokuwapo katika kituo hicho kuwa ni ukumbi wa mikutano, maktaba, huduma ya mtandao wa ‘internet’, ushauri nasaha na upimaji wa virusi vya ukimwi.
Chanzo: Tanzania Daima

0 comments:

 
Blogs za Mikoa
Copyright © 2012. Iringa Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa