Home » » MEYA CHADEMA, WENZAKE 5 KIZIMBANI

MEYA CHADEMA, WENZAKE 5 KIZIMBANI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Imeandikwa na Frank Leonard, Iringa
Meya wa Manispaa ya Iringa, Alex Kimbe
MEYA wa Manispaa ya Iringa, Alex Kimbe na wafuasi wenzake watano wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), wamepandishwa kizimbani mjini Iringa, kujibu mashitaka yanayohusishwa na vurugu za uchaguzi mdogo wa udiwani Kata ya Kitwiru, Iringa mjini.
Wakati Meya huyo aliachiwa jana kwa dhamana na Mahakama ya Wilaya Iringa, baada ya kusota rumande kwa siku tatu, Mahakama ya Hakimu Mkazi Iringa iliwanyima dhamana wafuasi hao watano kwa kuwa kati ya makosa matatu, wanayotuhumiwa kuyafanya kosa moja halidhaminiki.
Mwendesha Mashtaka wa Polisi, Aristeck Mwinyikheri alisema Kimbe aliyefikishwa mahakamani hapo kwa kesi Namba 189 ya mwaka 2017, anashitakiwa kutishia kumuua mtu kwa bastola katika tukio la Novemba 26, mwaka huu katika Kata ya Kitwiru mjini Iringa, wakati shughuli ya uchaguzi mdogo wa udiwani wa kata hiyo ikiendelea.
Mwinyikheri alisema Meya huyo alitenda kosa hilo kwa Alphonce Muyinga, ambaye ni Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM), kinyume na Kifungu Namba 89 (2) (a) cha Kanuni za Adhabu.
Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Wilaya ya Iringa, John Mpitanjia alisema shauri hilo litarudi tena mahakamani hapo Desemba 12, mwaka huu. Wakati huohuo, Mahakama ya Hakimu Mkazi Iringa imewanyima dhamana Martha Robert, Leonard Kulijira, Esau Bwire, Christopher Jevas na Samwel Nyanda, wafuasi wa Chadema ambao kwa pamoja wameshitakiwa mahakamani kupitia kesi namba 190 ya mwaka 2017 kwa makosa matatu.
Mbele ya hakimu mkazi wa Mahakama hiyo, Richard Kasele , Mwendesha Mashitaka wa Mahakama hiyo Chakila Felix alisema washitakiwa hao wafuasi wa Chadema, wanatuhumiwa kujeruhi, kuteka na kufanya unyang’anyi kwa kutumia nguvu.
Felix alisema watuhumiwa hao wanatuhumiwa kumjeruhi Dick Frank na kumnyang’anya simu yake ya mkononi. Mahakama hiyo imewarudisha rumande washitakiwa hao baada ya kunyimwa dhamana kwa kuwa kosa la unyang’anyi kwa kutumia nguvu, halina dhamana na shauri lao litarudi tena mahakamani hapo Desemba 12, mwaka huu.
CHANZO HABARI LEO

0 comments:

 
Powered by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Iringa Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa