Home » » Mpango wa elimu bure walete mafanikio Iringa.

Mpango wa elimu bure walete mafanikio Iringa.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Amina Masenza
Agizo la serikali la kutoa elimu bure kuanzia shule za msingi hadi kidato cha nne, limeanza kuonyesha matunda kwa baadhi ya shule kuwa na ongezeko kubwa la wanafunzi mkoani Iringa. 
 
Hayo yamebainika baada ya Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Amina Masenza,  juzi kutembelea na kukagua utekelezaji wa agizo hilo na changamoto zake. Katika ziara hiyo, alibaini ongezeko hilo limesababisha upungufu wa madarasa na madawati.
 
Akiwa katika shule za sekondari Kiwere, Kidamali na Kalenga, Masenza  aliarifiwa kuwapo na mwitikio mzuri wa wanafunzi kuripoti shuleni huku wale walioacha kutokana na kukosa, ada wakiomba kurejea.
 
Sixtus Kanyama, Mkuu wa Shule ya Sekondari Kidamali, alisema katika shule yake wameongezeka zaidi ya wanafunzi 100, hatua ambayo imesababisha kukaa wawili wawili. 
 
Naye Blandina Nkondola, mkuu wa shule ya sekondari Kiwere, alisema   fedha zilizotolewa na serikali kwa kila mwezi, hazitoshelezi mahitaji halisi ya msingi katika uendeshaji wa shule.
 
Hata hivyo,  mkuu huyo wa mkoa hakusita kutoa makucha yake kwa shule ambazo wanafunzi hawajaripoti kuanza kidato cha kwanza hadi sasa. Aliagiza watendaji wa kata wasioweza kutekeleza wajibu wao wajifikirie kama wanafaa kuendelea kuwamo katika nafasi zao.
 
Alisema kila mtendaji wa kijiji, atoe taarifa kwenye ofisi yake kwa kutoa idadi ya watoto katika kijiji chake ambao hawajaripoti shuleni na kupeleka taarifa kwa mtendaji wa kata.
 
Pia alitoa mwezi mmoja kwa shule ya Kidamali kukamilisha maabara kama agizo la serikali linavyotaka, huku akielekeza shule zote ziwe zimetatua tatizo la madawati ifikapo Mei, mwaka huu.
 
Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Iringa, Steven Mhapa, na Mkurugenzi wake, Pudenciana Kisaka, walisema changamoto hizo zimeanza kutatuliwa kwa kuanza kutengeneza madawati na kukamilisha ujenzi wa maabara.
 
CHANZO: NIPASHE

0 comments:

 
Blogs za Mikoa
Copyright © 2012. Iringa Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa