Home » » WAATHIRIKA WAPATIWA MBUZI

WAATHIRIKA WAPATIWA MBUZI



HALMASHAURI ya Wilaya ya Kilolo imetoa msaada wa Mbuzi 18 kwa waathirika wa ugonjwa wa ukimwi wa kikundi cha Matumaini kilichopo kijiji cha Kitumbuka, msaada wenye lengo la kuwaongezea mtaji katika kukuza uchumi wao na kuwaepusha na hali duni.

Akikabidhi Mbuzi hao wenye thamani zaidi ya shilingi Milioni 1 na nusu, katika maadhimisho ya siku ya Ukimwi duniani, iliyofanyika katika Kijiji cha Kitumbuka, mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo Bw. Joseph Muhumba amesema msaada huo utawawezesha waathirika hao kuendelea kuzihudumia familia zao.

Aidha Muumba amesema jamii inatapaswa kufahamu kuwa waathirika wa ugonjwa wa ukimwi wanauwezo wa kuchangia shughuli za maendeleo kwa kufanya kazi, huku akiwataka wananchi kutambua kuwa kupata maambukizi sio mwisho wa maisha.

Mwenyekiti wa kikundi cha Mshikamano, cha wanaoishi na Virusi vya ukimwi Bw. Leonard Chusi amesema msaada huo unaongeza imani kwao ya kuwa jamii inawajali, tofauti na awali jamii ilivyokuwa na tabia ya kunyanyapaa, jambo lililochangia baadhi yao kupoteza maisha kwa hofu.

Naye mratibu wa Ukimwi Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo Faraja Chaula amesema Wilaya hiyo ina asilimia 9.1 cha watu wanaoishi na Virus vya Ukimwi, na kuwa sababu kubwa ya tatizo hilo ni pamoja na jamii kuendekeza mila na destuli potofu zilizopitwa na wakati.

Bi. Chaula amesema pia tatizo la ulevi wa kupindukia na jamii kutotumia Kondomu kwa usahihi wakati wa kujamiiana ni sababu zinazochangia maambukizi mpya ya VVU na hivyo kuwepo na idadi kubwa ya waathirika wa ugonjwa huo wa Ukimwi.

0 comments:

 
Powered by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Iringa Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa