Home » » Watumishi wa Afya wadaiwa kukosa ujuzi

Watumishi wa Afya wadaiwa kukosa ujuzi



Na Oliver Richard, Iringa
IMEFAHAMIKA kuwa asilimia 67 ya watumishi wa sekta ya afya katika Manispa ya Iringa hawana elimu na ujuzi wa huduma rafiki kwa vijana, jambo linalosababisha kundi kubwa la vijana kukosa kupatiwa huduma hiyo muhimu.

Hayo yalielezwa na Mratibu wa Afya ya Uzazi na Mtoto mkoani hapa, Mariam Mohamed, katika maadhimisho ya Siku ya Afya ya Uzazi kwa Vijana mkoani hapa, yaliyoandaliwa na Shirika la Tiba na Utafiti barani Afrika (AMREF).

Mariam alisema athari kwa vijana wa miaka 10-20 kwa ugonjwa wa ukimwi (VVU) ni asilimia 14 kwa takwimu za mwaka 2010, ambapo asilimia 19 ya vijana hutumia huduma rafiki ya afya ya uzazi kwa vijana.

Alisema asilimia 7 ya vijana wanaotumia vituo na kupewa ushauri nasaha na upimaji wa virusi vya Ukimwi waligundulika kuwa na VVU, huku asilimia 67 ya watumishi wa afya wa Manispaa ya Iringa wakiwa hawana ujuzi wa huduma rafiki ya kutoa huduma hiyo kwa vijana. 

Aidha kuhusu janga la Ukimwi Mkoa wa Iringa, Mariam alisema mkoa huo una maambukizi kwa asilimia 15.7, huku taarifa za wajawazito wakiwa na maambukizi kwa asilimia 14.6 katika takwimu za mwaka 2010.

Akitoa sababu zinazochangia tatizo la ugonjwa wa ukimwi mkoani Iringa, Mariam alisema ni pamoja na kuendeleza mila na desturi ambapo asilimia 12.6 ya maambukizi husababishwa na ukeketaji kwa wanawake, huku unyanyasaji wa kijinsia ukiwa asilimia 35.

Alisema kwa upande wa wanaume wanaotahiriwa ni asilimia 34 pekee, huku asilimia 66 ya wanaume mkoani hapa wakiwa bado hawana desturi ya kutahiri, jambo linalochangia tatizo la ugonjwa wa ukimwi.

Naye Mratibu wa Afya ya Uzazi na Mtoto, Sezalia Andrew, alisema kukosekana kwa elimu ya afya ya uzazi kwa kundi hilo la vijana, kunasababisha ongezeko la mimba kwa wasichana na hivyo kuwepo kwa matukio ya vifo vya uzazi.

Kwa upande wake, Dk. Elizabeth Mapella, Mratibu wa Afya ya Uzazi kutoka Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, aliwataka vijana kujenga desturi ya kujisomea vitabu ili kupata elimu mbalimbali, ikiwa pamoja na kufika katika vituo vya afya kupata elimu ya afya ya uzazi.

Mwanafunzi wa Shule ya Msingi Ipogolo, Shamira Lupola, alisema vijana wengi wanashindwa kufika katika vituo vya afya kutokana na kutopewa fursa ya kusikilizwa.

Winfrida Kiwone, mwanafunzi wa Shule ya Sekondari Kihesa, alisema wazazi na walimu waone umuhimu wa kushirikiana katika malezi ya watoto pasipo kutegeana, kwani wote wana wajibu wa kumlea na kumlinda kijana asiingie katika janga la ngono.

Chanzo: Mtanzania

0 comments:

 
Blogs za Mikoa
Copyright © 2012. Iringa Yetu - All Rights Reserved
Designed by Blogs za Mikoa
Proudly powered by Blogs za Mikoa