Home » » Mafunzo ya kanuni za kilimo yaleta tija

Mafunzo ya kanuni za kilimo yaleta tija

KIKUNDI cha wakulima wa kijiji cha Mangalali, Iringa vijijini kimeongeza uzalishaji wa mahindi kutoka gunia nane hadi 20 kwa ekari, baada ya kupata mafunzo ya kanuni bora za hifadhi ya mazao.
Mafunzo hayo yamewawezesha kupunguza upotevu wa nafaka katika mchakato wa kuvuna hadi kuhifadhi. Mwenyekiti wa kikundi hicho, Emelita Singaile, alisema kikundi hicho chenye wanachama 184 wenye wastani wa ekari tano kwa kila mmoja, kilianzishwa mwaka 2003 kikiwa na wanachama 45 na sasa kinanufaika na kuona matunda ya kilimo kutokana na kusimamia kanuni za kilimo.
Singile alisema mafunzo hayo kupitia mradi husishi wa kupunguza upotevu wa nafaka katika mnyororo wa thamani wa zao la mahindi unaoratibiwa na taasisi ya maendeleo mijini na vijijini (Rudi), yalifadhiliwa na taasisi ya Mapinduzi ya Kijani Barani Afrika (AGRA) inayosaidiwa na Taasisi ya Rockefeller Foundation ya Marekani.
Akitoa taarifa kwa wawakilishi wa Rockefeller Foundation waliowatembelea wakulima hao hivi karibuni, Singaile alisema kwa kupitia mradi huo wamepata pia mafunzo ya kilimo bora cha mahindi na ya matumizi sahihi ya pembejeo za kilimo.
“Tunavuna kwa kutumia maturubai yanayosaidia kupunguza uwezekano wa mavuno kupata maambukizi ya sumu kuvu (aflatoxin) pamoja na punje kupotea,” alisema.
Alisema mahindi wanayovuna, wanahifadhi kwa kutumia mifuko isiyoingiza hewa (PICS na AgroZ bags), Kihenge cha Chuma (metal silo) na kifukofuko (Cacoon).
Meneja wa Rudi, Allan Ngakonda alisema teknolojia hizo za uhifadhi kwa pamoja zinalifanya zao hilo kuwa katika hali ya usalama kwa muda mrefu zaidi bila kutumia kemikali zozote na hivyo kusaidia kulinda afya za walaji.
Alisema kabla ya mradi kuja na matumizi ya teknolojia hizo, wakulima walikuwa wanapoteza asilimia kati ya 25 na 40 ya mazao wanayovuna.

0 comments:

 
Powered by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Iringa Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa