Home » » SOKO KUU IRINGA 1896 - 2016.

SOKO KUU IRINGA 1896 - 2016.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Soko kuu Manispaa ya Iringa.
Unapozungumzia soko ni kitu muhimu sana, kwani mji wowote ukikosa soko, unaelezwa haujakamilika.
Hiyo ndiyo hali iliyoko katika Manispaa ya Iringa, ambako kuna masoko kadhaa. 
 
Mwenyekiti wa Masoko ya Manispaa ya Iringa, Sturmi Fussy, anasema hali ya masoko kwa Manispaa ya Iringa ni nzuri kibiashara, kulinganisha na mwaka jana, kwa sababu vitu mbalimbali vinapatikana ndani ya sokoni.
 
Fussy ambaye ni mfanyabiashara wa bidhaa mbalimbali zikiwamo za ndani (dukani) na vyakula kama vie mchele, anasema mzunguko wa fedha ni wa wastani.
 
Anasema, biashara kwa jumla ipo kwa wastani unaowezesha kuendesha maisha ya wana - Iringa.
 
“Tunaweza kusema mzunguko wa fedha ni mzuri, kwa sababu kama bidhaa zinapatikana na zinanunuliwa kwa haraka mzunguko unakuwa safi, lakini kama bidhaa hazipatikani mzunguko nao unakuwa sio mkubwa,” Fussy anatoa tafsiri ya kibiashara.
 
Anasema wao wafanyabiashara walipendekeza vituo vya mabasi viwe karibu na masoko ili wasafiri wanaoingia na kutoka, waweze kununua bidhaa kwenye masoko hayo, lakini vituo hivyo vimekuwa mbali na eneo la soko.
 
Fussy anaongeza kuwa, Soko Kuu la Iringa limezungukwa na vituo vya kutolea huduma za kijamii kama vile Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Iringa, Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Magereza, Kituo cha Kikuu cha Polisi Iringa na kadhalika.
 
Anasema, iwapo kituo cha mabasi kingekuwa karibu na soko, watu wote wangenunua bidhaa sokoni, kwani wapo wanaonunua kwa ajili ya matumizi ya nyumbani na wengine kwa ajili ya kuuza.
 
Fussy anasema kuwa, hali ya biashara kwa mwaka jana na mwaka huu imekuwa tofauti, kwa sababu mwaka jana ulikuwa na ukame, tofauti na mwaka huu.
 
“Mfano mwaka jana mchele ulikuwa kwa kilo moja ulikuwa Sh 2400, lakini kwa mwaka huu kilo moja Sh.1900, ndio maana nikasema bora mwaka huu kuna neema kidogo kuliko mwaka jana. Hata hivyo, mvua zinaendelea kunyesha, naamini hata wakulima watalima mazao na chakula kitapatikana cha kutosha” anasema Fussy.
 
Anafafanua kuwa Manispaa ya Iringa ina masoko saba, ambayo ni Soko Kuu, Soko Dogo la Mshindo, Mashine Tatu, Mlandege, Magari Mabavu, Ipogolo na Kihesa.
 
Fussy anafanya ulinganishi akisema kuwa Soko la Mashine Tatu lina biashara nzuri kutokana na kuwa katika eneo lenye mzunguko mkubwa wa fedha.
 
Anafafanua kuwa, sababu kuu ni kwamba abiria wa mjini wanashukia Stendi Kuu ya Mabasi yaendeyo mikoani na kutumia fursa ya kununua vitu ndani ya soko hilo, pia lipo karibu na stendi.
 
HISTORIA YA SOKO
Mkuu wa Soko Kuu la Iringa, Michael Mage anasema historia yake ina mizizi mirefu katika zama zilizopita, Soko C, ambalo lilijengwa mwaka 1896, katika zama za utawala wa Kijerumani, likiwa na vizimba vichache kwa wakati huo.
 
Mage anasema kuwa hali hiyo iliendelea hadi mwaka 1972 ikiwa ni miaka 11 ya taifa kupata uhuru toka kwenye koloni la Waingereza, walipata sehemu ya kuongeza soko hilo, kukidhi mahitaji ya ongezeko kubwa la watu.
 
“Sehemu tulipopata soko jingine, awali ilikuwa stendi. Tukaamua kuwahamisha na kuweka soko jingine, ili kuweza kukidhi mahitaji ya watu na tulifanya hivyo kutokana na ongezeko la watu,” anasema Michael  .
 
Anasema sehemu iliyokuwa stendi, walijenga vizimba 176, baada ya kukabiliwa na ongezeko la watu mwaka 1972. Pia, mwaka 2009 ilifanyika ongezeko la vizimba.
 
Mage anasema kuwa, waliongeza wafanyabiashara 147 na ndio sababu ya kuonekana vioski nje ya soko na vizimba vipya ndani ya soko.
 
Mkuu huyo wa soko anasema kuwa, nafasi katika soko hilo imejaa na kinachofanyika ni kutangaza nafasi katika soko la Kihesa, Kitwiru,Ipogolo, Kitanzini, Mlandege.
 
CHANGAMOTO
Anasema changamoto wanayokumbana nayo ni pale anapowaambia wafanyabiashara kwenda kwenye masoko mengine, huwa wanagoma na kusema Soko Kuu ndio ‘Senta’ ya biashara na hivyo kufanya biashara zao kando ya soko au barabara.
 
Mage anasema changamoto nyingine, ni kwamba wafanyabiashara wanaendesha shughuli zao katika sehemu zisizo rasmi na ndicho kinachowafanya wenye vizimba kutouza bidhaa zao sana.
 
“Tutawafukuza leo, lakini kesho utakuta wamerudi. Ila sehemu za kuwahamishia tunazo na wao hawataki kwenda kwenye masoko hayo,” anasema Michael.
 
Aidha, anasema biashara kwa kipindi cha mvua ni ngumu, kutokana na biashara ya mali mbichi kuoza kutokana na kunyeshewa.
 
“Unaweza kuagiza mzigo wa matunda gari zima lakini mzigo huo unaishia jalalani kutokana na kuharibika. Mfano, matunda hayo yanaishia jalalani na unakuta mtu kaleta mzigo kabla ya kuingiza mezani, tayari asilimia kubwa umeshaharibika,” anasema 
Mage anasema, kwa sasa wamejipanga kuboresha masoko yao ili yawe ya kisasa hasa kwa masoko ya Kihesa na Mlandege, ili yakidhi mahitaji  ya wafanyabiashara wake.
 
KAULI YA WAFANYABIASHARA
Rajab Mtatifikolo, anayeuza viazi mviringo mjini Iringa, anasema mwezi Januari biashara haikuwa nzuri, kwa sababu sehemu kubwa ya bajeti ya wateja ilielekezwa kwenye mahitaji ya watoto wao.
 
Anasema, changamoto waliyokumbana nayo katika  kipindi cha nyuma, kunyanyaswa na askari mgambo wa Manispaa, hata kunyang’anywa na bidhaa zao za viazi kwa maana wao wamekuwa wakizunguka zunguka.
 
“Manispaa wanataka tuuze nje ya mji na nje ya mji ambako hakuna wanunuzi,wanunuzi wapo katikati ya mji, ndio maana wamekuwa wakituzungusha na sisi tunategemea bidhaa hii ya kutembeza viazi mviringo,” anasema Mtatifikolo.
 
Anasema bei za viazi zinatofautiana, kwani kuna viazi vinavyotoka mkoa wa Njombe, Mbeya na vingine ni vya Iringa na tofauti kuu inatokana na gharama za usafirishaji.
 
Mtafitikolo anataja bei zake kuwa, viazi vinavyotoka Mbeya gunia moja linauzwa Sh.70, 000; Njombe Sh.80, 000 na Iringa Sh. 65,000.
 
Anaeleza mtazamo wake kuwa, biashara itakuwa nzuri pale kipindi cha ununuzi wa vifaa vya wanafunzi kitapita na Mgambo wa Manispaa wataacha kuwanyanyasa, huku akisisitiza kuwa eneo la katikati ya mji ni muhimu kwao, kwani lina mzunguko mkubwa wa fedha. 
 
Bligitha Sulemani, anayeuza mchele katika soko la Mashine Tatu, anasema bei ya mchele inatofautiana kulingana ubora wake na nji kawaida katika kipindi  cha ukame bei ya mchele kupanda.
 
Anatoa mfano kuwa, mchele unaotoka mkoani Mbeya unapaswa kuuzwa kwenye Super Market, kwa sababu mauzo yake ni taratibu kutokan ana kuwa na bei kubwa.
 
Anaongeza kuwa, mchele unaotoka Iringa eneo la Pawaga, Idodi na Madibila ambao upo mpakani na Mbeya, bei zake ziko tofauti kuanzia Sh.1900 hadi Sh. 2400.
 
“Kwa sasa mchele hauwezi kushuka be, kwa sababu bado wakulima hawajavuna mpunga mashambani na watakapovuna mwezi wa sita, yawezekana ukashuka kwa maana kila eneo wanaingiza mchele mpya,” anasema Bligitha 
 
WANUNUZI NA WAUZAJI SOKO KUU
Wateja wa nyanya katika Soko Kuu la Iringa, wanalalamika kuwa wafanyabiashara wanawauzia nyanya kwa bei ghali kikiwa na kiwango cha chini, jambo linalofanya washindwe kununua bidhaa hizo.
 
Stella Aretasi ni mnunuzi anayeeleza kwa mfano kuwa, nyanya inauzwa kwa kibaba cha maji cha lita moja kwa bei ya Sh.1, 000 mtu akitaka kiwango cha chini cha nyanya ni Sh. 300 hawezi kupata kwa sababu wanauza kuanzia Sh.1000 na kuendelea.
 
Anaongeza kuwa inatakiwa wafanyabishara hao waweke bei ya chini hata kama mtu wa kiwango cha chini akitaka kununua nyanya moja ya Sh. 50 au Sh. 100 apate, lakini wakiuza kwa kibaba cha lita moja Sh. 1000 wanawaumiza watu wa kiwango cha chini.
 
Mfanyabiashara anayejitambulisha kwa jina la Baba Sharon, anayeuza samaki katika Soko kuu la Iringa, anasema bidhaa hiyo sasa haipatikani kirahisi, sababu ni kukosekana maji katika Bwawa la Mtera.
 
“Tumekosa samaki wakubwa, kwa sababu ya bwawa kukosa maji. Lakini tunawaomba watu wanaohusika na bwawa hilo wahakikishe kipindi hiki cha mvua, wanalijaza bwawa hilo maji ya kutosha ili samaki waendelee kuzaliana na kuwachukulia hatua kali za kisheria watu ambao wanaenda kukinga maji au kufungulia maji kwenye mashamba yao kwa ajili ya shughuli za kilimo,” anasema na kuongeza:
 
“Watu wa kiwango cha chini wakiona samaki wadogo  kama hawa wanawakimbilia kwa sababu tunauza bei ya chini, lakini sisi kama wafanyabishara hatupendi kuuza samaki wadogo ila inatubidi tu.”
 
Anahiyimisha kuwa, endapo maji yatakuwa yanapatikana ana imani kuwa samaki watazaliana kwa wingi na watakuwa na samaki wakubwa nao watapatikana, kuridhisha matakwa ya wateja wote
 
CHANZO: NIPASHE

0 comments:

 
Powered by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Iringa Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa