Home » » Kamati ya PAC yaridhishwa na Miradi ya REA

Kamati ya PAC yaridhishwa na Miradi ya REA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dkt. Merard Kalemani,(kushoto) akisalimiana na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Amina Masenza( kulia) mara baada ya kuwasili mkoani huo kwa ziara ya kukagua utekelezaji wa Miradi ya Umeme Vijijini katika Mkoa huo.
Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dkt. Merard Kalemani,(kulia) akisamilia na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali ( PAC), Livingstone Lusinde( kulia) walipowalisi mkoani wa Iringa, kwa ziara ya kukagua utekelezaji wa Miradi ya Umeme Vijijini mkoani huo.
Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dkt. Merard Kalemani,(kushoto) na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), Livingstone Lusinde( kulia) wasikiliza hoja za Wajumbe wa Kamati ya PAC, (hawapo pichani) kabla ya kuanza ziara ya kukagua utekelezaji wa Miradi ya Umeme Vijijini mkoani Iringa.
Wajumbe wa Kamati ya PAC, wakisikiliza taarifa ya Mkoa wa Iringa, kabla ya kuanza ziara ya kukagua utekelezaji wa MIRADI ya Umeme vijijini mkoani Iringa.
Wajumbe wa Kamati ya PAC,wakikagua Miradi ya Umeme Vijijini katika kijiji cha Nyamahana mkoani Iringa.
Mjumbe wa Kamati ya PAC, Shally Raymond( kulia) akisisitiza jambo kwa wanafunzi wa shule ya Sekondari Idodi, wakati wa ziara ya kukagua utelezaji wa Miradi ya Umeme Vijijini.
Mwenyekiti wa Kamati ya PAC, Livingstone Lusinde ( kushoto) akiruka pamoja na wanafunzi wa shule ya Sekondari Idodi, wakati wa ziara ya kukagua Miradi ya Umeme Vijijini.
Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dkt. Merard Kalemani,(kulia) akisalimiana na wanafunzi wa shule ya Sekondari Idodi, wakati wa ziara ya kukagua Miradi ya Umeme Vijijini.
………………………..
Na Zuena Msuya, Iringa

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) imeridhishwa na utekelezaji wa Miradi ya Umeme Vijijini, Unaotekelezwa na Wakala wa Nishati Vijijini (REA) katika Awamu ya kwanza na ya Pili ili kuona thamani halisi ya matumizi ya fedha za Serikali katika mradi huo.
Mwenyekiti wa PAC, Livingstone Lusinde alisema hayo mkoani Iringa wakati wa ziara ya kukagua utekelezaji wa mradi wa REA, katika vijiji na Taasisi mbalimbali zilizopitiwa na Mradi huo.

Lusinde alifafanua kuwa wameridhishwa na utekelezaji wa miradi hiyo baada ya kuona miundombinu iliyotumika na maendeleo ya wananchi katika maeneo ambayo yamepitiwa na miradi hiyo.

” Tumepita katika vijiji mbalimbali hapa Iringa ambayo nimepitiwa na REA,tumeona namna ambavyo mradi huo umetekelezwa na tumeona miundombinu iliyotumika na maendeleo yake hivyo hatuna budi kusema wazi kuwa tumeridhishwa na utekelezaji wa mradi huu”, Alisema Lusinde.

Lusinde aliwasisitiza wakandarasi wanaotekeleza Mradi wa Umeme vijijini, kutumia miundombinu imara inayokwenda sambamba na thamani halisi ya matumizi ya fedha za Serikali katika kutekeleza wa miradi hiyo ili kutimiza malengo yaliokusudiwa na kuondoa hasara za makusudi zinazoweza kujitokeza.


Vilevile aliwataka wakandarasi hao kukamilisha zoezi za kuwaunganisha na huduma ya umeme wananchi na Taasisi zilizoomba huduma hiyo katika maeneo machache yaliyosalia ili kila mwananchi aliyeomba huduma hiyo aweze kuipata kwa wakati na kuitumia.
Kwa upande wake Naibu Waziri wa Nishati na Madini DKt. Medard Kalemani alisema kuwa Awamu ya Tatu ya utekelezaji wa Mradi wa Umeme wa Vijijini utashirikisha Viongozi Serikali za mitaa, Madiwani,Wabunge, Wakuu wa Wilaya na Wakuu wa Mikoa.
Alifafanua kuwa lengo la kufanya hivyo ni kutoa fursa kwa wananchi kutoa vipaumbele vya maeneo wanayotaka kufikiwa kwa huduma ya umeme kwa wakati na kuvifikia vijiji vyote nchini.
” Mradi wa REA Awamu ya Tatu utakuwa shirikishi, kwakuwa kabla ya mkandarasi kuanza kazi yake, atatakiwa kuwasiliana na Viongozi wa Serikali ya mitaa, Madiwani, Wabunge , Wakuu wa Wilaya na Wakuu wa Mikoa ili wao watoe vipaumbe cha maeneo wanayotaka kufikiwa na mradi huo”, alifafanua Dkt. Kalema.
Dkt. Kalemani alibainisha kuwa utaratibu huo utawezesha kuviunganisha vijiji vyote nchini na huduma ya umeme ili kutimiza azma ya Serikali ya kufikia ya uchumi wa Kati ifikapo mwaka 2025.
Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali ( PAC) inafanya ziara ya kukagua Miradi ya Umeme Vijijini inayotekelezwa na Wakala wa Nishati Vijijini (REA)kwa kushirikiana na Shirika la Umeme Nchini ( Tanesco) kwa lengo la kuona thamani hali matumizi ya fedha ya Serikali katika mradi huo.

0 comments:

 
Powered by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Iringa Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa