Home » » Mbunge Kabati alaani kufungiwa kwa diwani wa viti maalum CCM Iringa mjini

Mbunge Kabati alaani kufungiwa kwa diwani wa viti maalum CCM Iringa mjini

 
 
Na MatukiodaimaBlog

MBUNGE  wa  viti  maalum  mkoa  wa Iringa Ritta  Kabati (CCM)  amepinga hatua ya mstahiki  meya  wa Manispaa  ya  Iringa Bw Alex Kimbe  kumsimamisha  vikao  vitatu diwani  wa  viti  maalum   Dolla Nziku (CCM) kwa madai ya  kuvunja kanuni  za  baraza la madiwani.

Mbali ya  kupinga uamuzi   huo wa Meya  mbunge  huyo amepongeza uamuzi  wa  waziri  wa ardhi , nyumba na maendeleo  ya makazi Bw  Wiliam  Lukuvi  kuzuia zoezi la Halmashauri  ya  Manispaa ya  Iringa  kuvunja  nyumba  za  watumishi ambao  wanadaiwa  kuwa ni makada wa CCM.

Akizungumza na wanahabari jana  mbunge  Kabati  alisema  kuwa Halmashauri ya Manispaa  ya Iringa ambayo  ipo  chini ya Chama  cha  Demokrasia  na maendeleo (CHADEMA)  imekuwa  ikiongozwa  kwa visasi jambo  ambalo linaweza  kurudisha  nyuma maendeleo ya  Halmashauri  hiyo.

Kwani  alisema kitendo cha Mstahiki  meya  huyo  kumondoa ndani ya kikao  cha  baraza la madiwani diwani Nziku  kwa  kutumia vijana  wa Chadema  ni  kosa la kikanuni na ni uvunjaji  wa kanuni  za vikao pia udhalilishaji  kwa  diwani  huyo  hivyo  kumtaka mstahiki  meya  kumwomba  radhi diwani  huyo.

Alisema  siku  ya  kikao   ambacho diwani  huyo  alisimamishwa kosa  lake  lilikuwa ni  kukosea  kuvaa kofia wakati wa kikao  kikiendelea  na ndipo  mstahiki  meya   huyo  alipoamua  kumfungia kuhudhuria  vikao  vya baraza la madiwani  hata  bila  kupewa  onyo ama kuitwa  kwenye  kikao  cha maadili .

“Kosa  alililitenda  halikuwa la  kumzuia  kushiriki  vikao  hivyo  bali  lilikuwa ni kosa la kuonywa pekee ila mbaya  zaidi meya  amekuwa akiendesha baraza la madiwani kama mkutano  wa Chadema  maana ndani ya baraza la madiwani hata kama  baraza  hilo  lipo chini ya Chadema ama  CCM haikupaswa vijana  wa chadema au  CCM kutumika kumwondoa diwani  ndani ya  kikao  cha kikanuni kwani  huo si  mkutano ama  kikao cha chama “

Kabati  alisema  kuwa muda  wa  kutumikia  adhabu ambao diwani  huyo  amepewa ni mkubwa na kutokana na kuwa  diwani  wa CCM kwa  viti maalum  kwenye Halmashauri   hiyo  yupo peke  yake kumpa  adhabu kubwa   hivyo ni  kuwanyima  wanawake kupata mwakilishi   wao ndani ya baraza   hilo .

Diwani  Nziku  alisema  kuwa  kofia   hiyo  ilianguka  bahati  mbaya   kutokana na nywele zake  kuvaa nywele  za bandia (wigi) hivyo  kofia  hiyo  kushindwa  kukaa kichwani na kuanguka  bila  kujua na baada ya  kuelezwa hakukaidi  aliivaa na  ndipo meya  huyo alipomtaka  kutoka nje  kwa kumpa  adhabu ya  kutoshiriki vikao vitatu .

“Sikukataa kutoka nje wakati nataka  kusimama kwenye kiti  ghafla meya  aliita mgambo  waje  kunitoa ila kabla ya mgambo  kufika vijana  wa Chadema  walinitoa kwa nguvu…..kweli  nilidhalilishwa   sana na  kitendo  hicho “

Katika  hatua  nyingine mbunge Kabati  alipongea uamuzi wa waziri  wa ardhi ,nyumba na maendeleo ya makazi Bw Lukuvi  kuzuia ukandamizaji  uliopangwa  kufanywa na Halmashauri  ya Manispaa ya  Iringa  chini ya Meya   huyo kuagiza  baadhi ya  nyumba za Halmashauri  wanazoishi  watumishi  wa umma hasa  wale  wanachama  wa CCM kuvunjwa kwa madai  ya  kutaka  kujenga mradi mkubwa .

Alisema  kuwa kabla ya  waziri  kufika   kuchukua uamuzi wa kusitisha  zoezi hilo  na  kuzichukua  nyumba  hizo  kutoka  serikali  za mitaa hadi  serikali  kuu  kuwa tayari uongozi wa Manispaa ya  Iringa  umesha  agiza makada hao wa CCM kuondoka katika  nyumba hizo na kuanza kuvunja  nyumba moja  eneo la Makorongoni kitendo  ambacho  kilimfanya  yeye mbunge  kufika  kupinga  uamuzi  huo.

Kwa  upande  wake Mstahiki  meya wa Maispaa ya  Iringa Bw  Kimbe  akijibu madai  hayo alisema  kuwa  kwa  suala la kupewa adhabu  diwani  huyo  lipo  kikanuni na hajafanya kwa matakwa  yake  ila  amezingatia taratibu na kanuni  zote  zinazompasa  kusimamia .

Bw  Kimbe  alisema  kuwa  kutokana na diwani  huyo kuvunja kanuni nay eye akiwa ni msimamizi wa kanuni  alimpa adhabu kwa  mujibu wa kanuni na kuwa adhabu  hiyo haina hata  chembe  ya chuki .

Pia  meya  huyo  alikanusha madai ya mbunge Kabati  kuwa zoezi la kuvunja nyumba  hizo liliwalenga wana CCM kwani  alisema zoezi hilo lililenga  nyumba tano bila  kuangalia anayeishi katika nyumba  hizo ni mwanachama wa chama gani  kwani kimsingi nyumba   hizo zilikuwa ni mali ya Halmashauri kwa ajili ya  watumishi  wake na  sababu ya  kutaka  kuzivunja ni  kuongeza  eneo la gulio katika  eneo  hilo .

Hata  hivyo alipongeza hatua ya waziri mwenye  dhamana ya  ardhi ,nyumba na maendeleo ya makazi  kumaliza  mgogoro  huo kwa nyumba  hizo na nyingine  zote  katika Halmashauri za  wilaya zaidi ya tano nchini  kuchukuliwana serikali  kuu.
MWISHO

Picha ;  Mbunge wa viti  maalum mkoa wa Iringa Bi  Ritta kabati wa  pili  kulia akitazama moja kati ya  nyumba za Halmashauri ya Manispaa ya  Iringa iliyovunjwa wengine ni wananchi  wa  kata ya Makorongoni ambao  baadhi yao  walipewa agizo la kuhama katika nyumba  za Halmashauri baada ya  kuagizwa  zivunjwe kwa madai ya  kulipa  kisasi na  kulia  wa kwanza  diwani wa viti maalum Dolla Nziku (CCM) ambae  kwa  sasa amesimamishwa kwa vikaa vitatu (picha na MatukiodaimaBlog )

0 comments:

 
Powered by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Iringa Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa