Home » » Wapewa elimu kumaliza migogoro ya ardhi

Wapewa elimu kumaliza migogoro ya ardhi

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

INAELEZWA kuwa migogoro ya ardhi itapungua katika maeneo mengi nchini, baada ya wajumbe wa Kamati za Uamuzi za vjiji 10 vya wilaya za Kilolo na Mufindi kupewa mafunzo ya haki za ardhi na utawala.
Ofisa Mradi wa Pelum Tanzania, Angole Rayson alisema mjini hapa juzi kuwa, walibaini kuwa migogoro mingi inasababishwa na ukosefu wa mbinu bora za kutatua migogoro ya ardhi pamoja na waamuzi kuwa na changamoto ya ufahamu wa masuala yanayohusu haki za ardhi na utawala.
Kwa mujibu wa Rayson, mafunzo hayo yaliyolenga kuwaongezea uelewa waamuzi hao kuhusu sheria za ardhi, haki za ardhi kwa wanawake na makundi maalumu, yatasaidia kuhakikisha wananchi wanapata haki katika masuala yote ya ardhi katika vijiji ambavyo waamuzi wake waliokwenye Kamati za uamuzi wamepata mafunzo hayo.
Alivitaja vijiji hivyo kuwa ni Ikuka, Mbigili, Mawala, Mawambala na Masalali kwa upande wa wilaya ya Kilolo na Isaula, Magunguli, Makungu, Usokami na Ugesa kwa upande wa wilaya ya Mufindi.
Mafunzo hayo yaliyofanywa kwa siku nne katika kila wilaya yametolewa na mtandao wa Mashirika yasiyokuwa ya Kiserikali yanayofanya kazi na wakulima na wafugaji wadogo nchini Tanzania (Pelum Tanzania).
Alisema mafunzo hayo yanatolewa kupitia mradi wa kuhusisha jamii ya vijijini katika uwajibikaji wa masuala ya ardhi ya kijiji unaojulikana kwa jina la CEGO unaotekelezwa kwa uratibu wa mtandao huo na ufadhili kutoka Shirika la Kimataifa la Maendeleo la Marekani (USAID).
Kwa maelezo yake, mradi huo wa miaka minne ulianza kutekelezwa mwaka 2013 ukihusisha pia vijiji vingine 20 vya wilaya nne katika mikoa ya Morogro na Dodoma.
“Shughuli kuu za mradi huo ni kuongeza na kuimarisha uelewa wa haki za ardhi kwa wananchi wa vijijini pamoja na viongozi wao kupitia mafunzo, machapisho na mijadala mbalimbali,” alisema.
Akifunga mafunzo hayo wilayani Mufindi, Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi, Isaya Mbenje alisema ardhi ni mojawapo ya rasilimali muhimu kwa maendeleo ya kijamii na kiuchumi katika nchi.

CHANZO GAZETI LA HABARI LEO

0 comments:

 
Powered by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Iringa Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa