Home » » Huduma za madaktari bingwa zaanza kutolewa mkoani Iringa

Huduma za madaktari bingwa zaanza kutolewa mkoani Iringa

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

Mganga Mkuu wa Serikali, Profesa Muhammad Kambi
WIZARA ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imezindua huduma za madaktari bingwa katika Hospitali ya mkoa wa Iringa sambamba na kampeni inayohamasisha utoaji kipaumbele cha huduma kwa wazee.
Huduma za madaktari hao zilizoanza kutolewa Aprili 25, mwaka huu zinahusisha magonjwa ya ndani ya moyo, usingizi na magonjwa mahututi, upasuaji, mfumo wa mkojo, watoto na magonjwa ya akinamama na uzazi.
Taarifa iliyotolewa na Mganga Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk Robert Kasim inaonesha tangu huduma za madaktari hao zianze kutolewa wagonjwa 245 wenye matatizo mbalimbali ya kiafya, wameonwa.
Dk Kasim alisema kati yao, 127 ni wanachama wa Mfuko wa Bima ya Afya (NHIF) kutoka maeneo mbalimbali ya mkoa huo na 118 ni wananchi wengine ambao si wanachama wa mfuko huo.
Akizindua huduma na kampeni hiyo juzi, Mganga Mkuu wa Serikali, Profesa Muhammad Kambi alisema mpango wa kupeleka madaktari bingwa mikoani ni moja ya mipango itakayoendelezwa ili kuhakikisha kila mwananchi anapata huduma bora za matibabu karibu na alipo.
“Huduma hizi tunazozitoa kwa kushirikiana na Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya tunazitoa hapa Iringa na zitaendelea kwa siku nyingine tano, huduma hizi zinahitaji fedha nyingi. Fedha hizo ni zile zinazochangwa na wanachama wa mfuko huo na zile za wanachama wa Mfuko wa Afya ya Jamii,” alisema.
Profesa Kambi alimweleza Katibu Mkuu wa wizara hiyo kuwa, pamoja na huduma hizo kupelekwa mkoani humo, takwimu zinaonesha wananchi wengi bado hawajachangamkia kujiunga na mifuko hiyo kwa kuzingatia taratibu mbalimbali za uchangiaji.
Akizungumzia huduma kwa wazee, alisema kwa kuwa wizara hiyo imepewa jukumu la kusimamia masuala ya wazee, wameona waanze kuwaenzi kwa kuhakikisha wanapata kipaumbele cha huduma za matibabu.
Awali Mkurugenzi wa Tiba na Ushauri wa Kiufundi wa NHIF, Frank Lakey alisema msingi mkubwa wa mpango huo ni dhamira ya NHIF ya kutoa huduma bora za matibabu kwa usawa kwa wanachama wake wote na wananchi kwa kuzingatia mahitaji yao, bila kujali hadhi zao, kiwango cha uchangiaji au maeneo ya kijiografia wanayoishi.
“Tangu kuanza kwa mpango huu mwaka 2013, mikoa 14 imefikiwa hadi sasa ambako wagonjwa 11,612 walipata huduma na kati yao 392 walifanyiwa upasuaji wa aina mbalimbali,” alisema kwa niaba ya Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa NHIF, Michael Mhando.
Awali Katibu Tawala wa Mkoa wa Iringa, Wamoja Ayubu aliipongeza wizara na NHIF kwa kubuni mpango huo unaosaidia kupunguza gharama kwa wagonjwa.

Chanzo Gazeti la Habari leo

0 comments:

 
Powered by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Iringa Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa