Home » » JAJI MFAWIDHI ASISITIZA JUKUMU LA MAHAKAMA.

JAJI MFAWIDHI ASISITIZA JUKUMU LA MAHAKAMA.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
JAJI Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Iringa, Mary Shangali amesema Mahakama kwa kushirikiana na wadau wake wengine ina jukumu la kutoa elimu ya sheria kwa umma ili uelewe taratibu za msingi katika upatikanaji wa haki mahakamani.
Akifungua rasmi Wiki ya utoaji wa elimu ya Sheria kwa umma katika viwanja vya Mahakama Kuu Kanda ya Iringa juzi, Jaji Shangali alisema Mahakama ya Tanzania imeazimia kuweka utaratibu wa kuadhimisha Siku ya Sheria nchini kwa kutanguliwa na Wiki ya elimu ya Sheria kwa wananchi.
Alisema utaratibu huo ulioanza jana, unawahusisha wadau wote katika sekta ya utoaji haki wakiwemo mawakili wa serikali, mawakili wa kujitegemea, Polisi, Magereza, Takukuru na vyama vya msaada wa kisheria.
Mbali na kutumia vituo vya redio kutoa elimu hiyo, Jaji Shangali alivitaja vituo vitakavyotumika pia kutoa elimu hiyo kuwa ni pamoja na kwenye magereza yote ya kanda ya Iringa, Jumba la Maendeleo mjini Iringa, Mahakama Kuu na viwanja vya manispaa.
Alisema wananchi wengi hasa wale wa vijijini watanufaika na utaratibu huo kwa kuzingatia kwamba wengi wao hawajui sheria na taratibu zinazotumika katika utoaji wa haki.
“Tunategemea wananchi wengi watajitokeza katika vituo hivyo ili wapate uelewa wa huduma zitolewazo na Mahakama na elimu ya Sheria kwa ujumla,” alisema Jaji Shangali.
 CHANZO; HABARI LEO.

0 comments:

 
Powered by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Iringa Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa