Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
JESHI la Polisi Mkoa wa Iringa limewatia mbaroni wahamiaji haramu 83,
raia wa Ethiopia, waliokuwa wakisafirishwa na gari aina ya Scania lenye
namba za usajili T478 DFE mali ya Frola Mwambenja, ambao walikuwa
wakitokea Kongowe jijini Dar es Salaam kuelekea Kyela mkoani Mbeya.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa jana, Kamanda wa Polisi
wa Mkoa wa Iringa, Peter Kakamba, alisema jeshi hilo linamshikilia pia
dereva wa gari hilo, Hans Mwakyoma (28) mkazi wa Tukuyu Mbeya na
msaidizi wake Alex Adam (32) mkazi wa Mbeya mjini, kwa tuhuma za
usafirishaji wa watu hao.
Kamanda Kakamba alisema gari hilo lilikamatwa na askari wa doria wa
jeshi hilo saa 3.30 usiku katika Kijiji cha Mahenge, barabara kuu ya
Iringa Mbeya likiwasafirisha watu hao kuelekea Kyela ambako ni mpakani
mwa Tanzania na Malawi.
“Lilipokamatwa roli hilo, dereva alisema halina mzigo, lakini askari
wetu walipolifungua walikuta watu hao wakiwa wamelaliana, baadhi yao
wakiwa na hali mbaya na wengine wakiwa wagonjwa,” alisema.
Alisema baada ya kuwakamata, wahamiaji hao walipewa chakula na wale
walioonekana wagonjwa wamepatiwa matibabu wakati taratibu zingine za
kuwafikisha katika vyombo vya sheria zikiendelea.
“Jambo la kushangaza ni kwamba watu hao walipakiwa katika gari hilo
Kongowe jijini Dar es Salaam. Kila mtu anajua Kongowe si Ethiopia kwa
hiyo kuna swali la kujiuliza ni namna walivyofika Kongowe hadi wakapata
huduma ya kusafirishwa kuelekea wanakoelekea,” alisema.
Alisema biashara haramu ya usafirishaji watu ni jipu kubwa
linalohitaji nguvu ya pamoja katika kulitumbua kwani inahusisha mtandao
wa watu wengi ndani na nje ya nchi.
Alisema katika kupambana na biashara hiyo, taarifa za kiintelejensia
za jeshi hilo zinaelekea kuunasa mtandao wa biashara hiyo na mkakati huo
utakapofanikiwa wahusika wake watatumbuliwa majipu hadharani.
Alisema watu hao wamekuwa wakiitia gharama kubwa serikali, kwani
baada ya kuwakamata imekuwa ikilazimika kuwahudumia na kuwasafirisha
hadi walipotoka.
CHANZO: MTANZANIA.
0 comments:
Post a Comment