Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa akihutubia mkutano wa
hadhara uliofanyika katika Viwanja vya Mwembetogwa, Iringa jana.
Mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa jana alisimamisha
kwa muda, shughuli za maelfu ya wakazi wa jimbo hilo ambao walijitokeza
kumsikiliza katika mkutano wa hadhara wa kuwashukuru ambao aliutumia
kuelezea mafanikio aliyopata katika kipindi cha miaka mitano ikiwamo ya
kuwafanya wajue haki zao.
Msigwa ambaye alitumia
mkutano huo kuomba ridhaa ya kuteuliwa na chama chake kugombea tena
ubunge alisema kitendo chake cha kuwaelimisha wananchi juu ya haki zao
ndicho kilichosababisha wakazi wa Mji wa Iringa kutowaogopa polisi wala
wakuu wa wilaya kama ilivyokuwa zamani.
“Ipo tofauti
kati ya kiongozi na mwanasiasa, kiongozi ni yule ambaye mambo yake
yanafikiria karne lakini mwanasiasa yeye hufikiria uchaguzi pekee, mtu
anayefikiria masuala ya muda mrefu anawekeza kwa watu… ndiyo sababu leo
wakazi wa Iringa wamejua haki zao,” alisema.
“Katika
kipindi cha miaka mitano tulilia pamoja na kucheka pamoja, wengi
wanakumbuka nilipowasaidia Machinga pale Mashine Tatu, tulikamatwa
pamoja na kuwekwa ndani pamoja, mbunge gani anaweza kukubali kulala
ndani kwa ajili ya watu wake? Nilifanya vile si kwa sababu sikuwa na
mahali pazuri pa kulala, bali nilitaka watu mpate haki zenu kwa kuwa
mimi niligombea nikitaka kuwa sauti ya wanyonge.”
Msigwa
alisema kutokana na uelewa huo, wakazi wa Iringa waligoma kuchangia
michango ya Mbio za Mwenge... “Nilipokuja kuwaambia hakuna kuchagia
Mbio za Mwenge, nani alichangia hapa?.... (hakuna) nani alikamatwa kwa
ajili ya kukataa kuchangia mchango huo? (hakuna) hiyo ni miongoni mwa
kazi kubwa niliyoifanya.” Alisema yeye na wabunge wenzake wamefanikiwa
kwa kiwango kikubwa kupandisha hadhi na heshima ya Bunge tofauti na
mabunge yaliyopita kutokana na kujituma kwao kuwatumikia wananchi...
“Tulikwenda bungeni tukakuta wabunge wanalala, tumewaamsha, hawasomi
tumewafanya wanasoma, wanaogopa Serikali tumewafanya hawaogopi hata
baadhi ya wabunge wa CCM kuthubutu kuikosoa Serikali yao.”
Alisema
Taifa limebaki katika dimbwi la umaskini kutokana na kuongozwa na
wanasiasa ambao wanafikiria uchaguzi na si masuala ya muda mrefu ya nchi
na ndiyo sababu Rais Jakaya Kikwete alitumia takriban saa mbili
kuzungumzia miradi wakati wa hotuba yake ya kuhitimisha Bunge.
“Leo
hii tunamkumbuka Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere siyo kwa sababu
alijenga daraja ama uwanja ni kwa kazi yake ya kuwekeza kwa watu na
ndiyo sababu sote tunakubali kuwa ni Baba wa Taifa,” alisema.
Achangiwa Sh5.1 milioni
Wananchi
waliohudhuria mkutano huo walichanga Sh5.1 milioni ambazo zilitangazwa
kwenye mkutano huo na Mkurugenzi wa Taasisi ya Ufuatiliaji Shughuli za
Bunge ya Chadema, Marcossy Albanie ambaye alisema ni kwa ajili ya
kuchukulia fomu.
Mke wa Msigwa hadharani
Kwa
mara ya kwanza, mke wa mbunge huyo, Kissa Msigwa alisimama jukwaani na
kutoa shukrani kwa wakazi wa Iringa kwa kumpa nafasi ya uwakilishi
mumewe.
Huku akishangiliwa Kissa alisema:
“Ninawashukuru wakazi wa Iringa kwa kumchagua... amewakilisha vizuri
naomba mmpatie tena miaka mitano ili aweze kuifanya kazi hiyo.”
Mbunge
wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi ambaye aliongozana na Msigwa alitumia
muda mwingi kwa mgombea urais wa CCM, Dk John Magufuli akisema hataweza
kupambana na nguvu ya Ukawa itakayoongozwa na Katibu Mkuu wa Chadema, Dk
Willbrod Slaa.
Mbilinyi alisema hivi karibuni Ukawa itatangaza mgombea urais huku akisema Dk Slaa ni jembe.
Kuhusu
Msigwa, Mbilinyi alisema ni miongoni mwa wabunge ambao Iringa na Taifa
linawategemea na kuwaomba wakazi wa Iringa Mjini kutompoteza.
Katibu
wa Baraza la Wanawake wa Chadema (Bawacha ), Grace Tendega alisema
upinzani utaibuka na ushindi mwaka huu... “Kama mnavyoona katika majimbo
ya Monduli na Bariadi, hali hiyo bado na itaendelea nchi nzima, watu
wamechoshwa na CCM na sasa wameamua kuja Chadema na muda si mrefu
tutatangaza mgombea mtamuona na atashinda Uchaguzi Mkuu mwaka huu.”
Mwenyekiti
wa Chadema Iringa Mjini, Frank Nyalusi alisema: “Katika kipindi cha
uongozi wake, Msigwa miradi mingi ya maendeleo imetekelezwa.”
Chanzo:Mwananchi
Chanzo:Mwananchi
0 comments:
Post a Comment