Home » » MSIGWA ASIMAMISHA SHUGHULI IRINGA

MSIGWA ASIMAMISHA SHUGHULI IRINGA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
 Mbunge wa Iringa  Mjini, Mchungaji Peter Msigwa Mbunge wa Iringa  Mjini, Mchungaji Peter Msigwa akihutubia mkutano wa hadhara uliofanyika katika Viwanja vya Mwembetogwa, Iringa jana.

Mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa jana alisimamisha kwa muda, shughuli za maelfu ya wakazi wa jimbo hilo ambao walijitokeza kumsikiliza katika mkutano wa hadhara wa kuwashukuru ambao aliutumia kuelezea mafanikio aliyopata katika kipindi cha miaka mitano ikiwamo ya kuwafanya wajue haki zao.
Msigwa ambaye alitumia mkutano huo kuomba ridhaa ya kuteuliwa na chama chake kugombea tena ubunge alisema kitendo chake cha kuwaelimisha wananchi juu ya haki zao ndicho kilichosababisha wakazi wa Mji wa Iringa kutowaogopa polisi wala wakuu wa wilaya kama ilivyokuwa zamani.
“Ipo  tofauti kati ya kiongozi na mwanasiasa, kiongozi ni yule ambaye mambo yake yanafikiria karne lakini mwanasiasa yeye hufikiria uchaguzi pekee, mtu anayefikiria masuala ya muda mrefu anawekeza kwa watu… ndiyo sababu leo wakazi wa Iringa wamejua haki zao,” alisema.
“Katika kipindi cha miaka mitano tulilia pamoja na kucheka pamoja, wengi wanakumbuka nilipowasaidia Machinga pale Mashine Tatu, tulikamatwa pamoja na kuwekwa ndani pamoja, mbunge gani anaweza kukubali kulala ndani kwa ajili ya watu wake? Nilifanya vile si kwa sababu sikuwa na mahali pazuri pa kulala, bali nilitaka watu mpate haki zenu kwa kuwa mimi niligombea nikitaka kuwa sauti ya wanyonge.”
Msigwa alisema kutokana na uelewa huo, wakazi wa Iringa waligoma kuchangia michango ya Mbio za Mwenge... “Nilipokuja  kuwaambia hakuna kuchagia Mbio za Mwenge, nani alichangia hapa?.... (hakuna) nani alikamatwa kwa ajili ya kukataa kuchangia mchango huo? (hakuna) hiyo ni miongoni mwa kazi kubwa niliyoifanya.” Alisema yeye na wabunge wenzake wamefanikiwa kwa kiwango kikubwa kupandisha hadhi na heshima ya Bunge tofauti na mabunge yaliyopita kutokana na kujituma kwao kuwatumikia wananchi... “Tulikwenda bungeni tukakuta wabunge wanalala, tumewaamsha, hawasomi tumewafanya wanasoma, wanaogopa Serikali tumewafanya hawaogopi hata baadhi ya wabunge wa CCM kuthubutu kuikosoa Serikali yao.”
Alisema Taifa limebaki katika dimbwi la umaskini kutokana na kuongozwa na wanasiasa ambao wanafikiria uchaguzi na si masuala ya muda mrefu ya nchi na ndiyo sababu Rais Jakaya Kikwete alitumia takriban saa mbili kuzungumzia miradi wakati wa hotuba yake ya kuhitimisha Bunge.
“Leo hii tunamkumbuka Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere siyo kwa sababu alijenga daraja ama uwanja ni kwa kazi yake ya kuwekeza kwa watu na ndiyo sababu sote tunakubali kuwa ni Baba wa Taifa,” alisema.
Achangiwa Sh5.1 milioni
Wananchi waliohudhuria mkutano huo walichanga Sh5.1 milioni ambazo zilitangazwa kwenye mkutano huo na Mkurugenzi wa Taasisi ya Ufuatiliaji Shughuli za Bunge ya Chadema,  Marcossy Albanie ambaye alisema ni kwa ajili ya kuchukulia fomu.
Mke wa Msigwa hadharani
Kwa mara ya kwanza, mke wa mbunge huyo, Kissa Msigwa alisimama jukwaani na kutoa shukrani kwa wakazi wa Iringa kwa kumpa nafasi ya uwakilishi mumewe.
Huku akishangiliwa Kissa alisema: “Ninawashukuru wakazi wa Iringa kwa kumchagua... amewakilisha vizuri naomba mmpatie tena miaka mitano ili aweze kuifanya kazi hiyo.”
Mbunge wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi ambaye aliongozana na Msigwa alitumia muda mwingi kwa mgombea urais wa CCM, Dk John Magufuli akisema hataweza kupambana na nguvu ya Ukawa itakayoongozwa na Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willbrod Slaa.
Mbilinyi alisema hivi karibuni Ukawa itatangaza mgombea urais huku akisema Dk Slaa ni jembe.
Kuhusu Msigwa, Mbilinyi alisema ni miongoni mwa wabunge ambao Iringa na Taifa linawategemea na kuwaomba wakazi wa Iringa Mjini kutompoteza.
Katibu wa Baraza la Wanawake wa Chadema (Bawacha ), Grace Tendega alisema upinzani utaibuka na ushindi mwaka huu... “Kama mnavyoona katika majimbo ya Monduli na Bariadi, hali hiyo bado na itaendelea nchi nzima, watu wamechoshwa na CCM na sasa wameamua kuja Chadema na muda si mrefu tutatangaza mgombea mtamuona na atashinda Uchaguzi Mkuu mwaka huu.”
Mwenyekiti wa Chadema Iringa Mjini, Frank Nyalusi alisema: “Katika kipindi cha uongozi wake, Msigwa miradi mingi ya maendeleo imetekelezwa.”
Chanzo:Mwananchi

0 comments:

 
Powered by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Iringa Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa