Home » » MGIMWA: AIBU WATOTO WETU KUFANYA KAZI ZA NDANI

MGIMWA: AIBU WATOTO WETU KUFANYA KAZI ZA NDANI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
 
MBUNGE wa Kalenga mkoani Iringa Godfrey Mgimwa amewataka wazazi kuacha tabia ya kuwapeleka watoto wao waliohitimu darasa la saba kufanya kazi za ndani mijini kwa kuwa ni aibu kwa wakazi wa mkoa huo.
Akizungumza katika mahafali ya darasa la saba katika shule ya msingi Kalenga na Kiponzelo juzi mbunge Mgimwa alisema kuwa mkoa wa Iringa umekuwa ukisifika kwa kutoa wafanyakazi wa ndani jambo ambalo ni aibu na asingependa jimbo lake kuwa katika orodha ya yanayosifika kwa hilo.
Mbunge huyo, alisema kwa muda ambao atakuwepo madarakani kama mbunge, atafurahi kuona wazazi wanawasomesha watoto wao elimu ya Sekondari ama ufundi ili kuja kuwasaidia mbeleni, badala ya kuwaruhusu kwenda mijini kutumikishwa kazi za ndani na kwenye madanguro, ambako yanaweza kuwasababishia kurudi kijijini na maambukizi ya virusi vya Ukimwi.
"Wazazi wa wanafunzi wanaomaliza darasa la saba katika shule zote za msingi jimbo langu la Kalenga, ninaomba sana kuungana katika kulijenga jimbo kwa kutowaruhusu watu wenye nia mbaya kuja kukusanya watoto wetu na kuwapeleka mijini katika kazi za ndani na madanguro," alisema.
Alisema kitendo cha baadhi ya wazazi kutopenda kuwasomesha watoto elimu ya sekondari na kuwaruhusu kwenda kufanya kazi ya ndani si heshima kwa  Kalenga na mkoa mzima, bali ni aibu kubwa ambayo kama isipo kemewa itajenga dhana ya kuwa Iringa ni kisima cha wafanyakazi wa ndani.
  Mgimwa alisema kuwa umefika wakati kwa wakazi wa Iringa kuungana pamoja na kuugeuza mkoa huo kuwa wa maendeleo badala ya kuwa wa kuzalisha wafanyakazi wa ndani.
Katika mafahali hayo, Mgimwa alijitolea kusaidia ujenzi wa choo cha wanafunzi katika shule ya Msingi Kalenga kwa kutoa fedha za kununua bati  43 pamoja na kusaidia ujenzi wa vyoo vya matundu 18 ya wanafunzi katika shule ya msingi Kiponzelo.
 Chanzo:Tanzania Daima

0 comments:

 
Powered by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Iringa Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa