Home » » ELIMU HAIKUWA KIKWAZO KATIKA MAISHA YANGU

ELIMU HAIKUWA KIKWAZO KATIKA MAISHA YANGU

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
 
Jina la Madaraka Kilangi (52) kwa wenye malori makubwa aina ya Scania Kanda ya Nyanda za Juu Kusini lipo mdomoni.
Ni fundi na muuzaji maarufu wa vipuri vya magari hayo kwa miaka 30, ni mtu mwenye historia fupi, lakini yenye kuvutia.
Kilangi mwenye elimu ya darasa la saba aliyoipata katika Shule ya Msingi Mwembetogwa mjini Iringa, kwa sasa ni mfanyakazi na mmiliki wa kampuni tatu zenye majina makubwa jijini Mbeya.
Anamiliki Kampuni za Madaraka Auto Garage, Lulu Auto Spares na Mbeya Spring drinking Water and Kilangi Investiment Company Limited. “Mimi nina elimu ya darasa la saba, Mungu amenipa madaraka ya kuthubutu na hatimaye kumiliki mali ingawa siyo tajiri, kwani mbali ya kampuni zangu, pia ninamiliki nyumba 10 za kupangisha na magari mawili ya kunyanyua magari mazito yaliyoanguka,’’ anasema.
Kilangi akiwa amevalia koti la bluu la kikazi zaidi akiwa katika gereji yake, anasema siri ya mafanikio yake ni kujituma na uaminifu.
“Baada ya kumaliza elimu ya msingi niliomba kibarua kwenye Kampuni ya Maliki Auto Garage na pale nilifanya kazi kwa bidii na kujifunza mambo mengi,’’ anasema Kilangi.
Anasema baada ya miaka 14 kwenye gereji hiyo, alinunua kiwanja kwa Sh100,000 na kuanzisha gereji yake ndogo ambayo aliipa jina la Madaraka Auto Garage.
“Hapa nilikuwa na vijana niliowafundisha kazi na wengi wao kwa sasa wana gereji kubwa katika Jiji la Dar es Salaam, Iringa na hata hapa Mbeya,’’ anasema.
Kilangi mwenye wake wawili, anasema baada ya muda alifungua duka la kuuza vipuri vya magari aina ya Scania pekee. “Mimi naamini umasikini ni matokeo ya uoga katika kuthubutu, kwani mimi nilithubutu kukopa fedha nyingi benki licha ya riba kuwa kubwa, lakini walau nilipata mtaji ambao nazunguka nao mpaka sasa.’’
Anatoa mfano wa riba kuwa kubwa kwamba mtu akikopa Sh200 milioni benki atarudisha jumla ya Sh350 milioni, ikiwamo riba ya Sh150 milioni. Kilangi anasisitiza umuhimu wa mtu anayekopa kuwa na malengo ili aweze kufanikiwa na kusema hofu yake kwa sasa ni mtazamo mbaya wa vijana wanaomaliza vyuo vikuu wanapotafuta kazi.
“Pamoja na kwamba mimi ni mkurugenzi mkuu, lakini nauza duka langu, nashika spana na kuhangaika na kazi zote za kampuni. Nashindwa kuwaamini vijana wanaohitimu vyuo vikuu hapa nchini, kwa sababu hawatabiriki. Hawana ari na kazi, wanafikiria zaidi kuiba tofauti na vijana wasomi kutoka Zambia, Kenya au Uganda ambao wakipata kazi wanafanya kwa bidii,’’ anasema.
Itaendelea Alhamisi ijayo
 Chanzo;Mwananchi

0 comments:

 
Powered by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Iringa Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa