Home » » VIFAA VYA SETELAITI KUSIMAMIA TEMBO WOTE

VIFAA VYA SETELAITI KUSIMAMIA TEMBO WOTE

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

TEMBO wa Hifadhi ya Taifa ya Ruaha iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Iringa Vijijini, watafungwa kifaa maalumu cha kufuatilia mwenendo wa wanyama hao ambao wapo katika kasi kubwa ya kutaka kutoweka kwenye ramani za hifadhi.
Hatua hiyo inatokana na ujangili unaoendelea ambapo vifaa hivyo vinakuwa kwenye harakati za ziada za serikali na wadau wake za kuwanusuru wanyama hao na majangili wa meno yake.
Mpango huo utakaotumia teknolojia ya kisasa ya mawasiliano ya satelaiti ya utambuzi wa jiografia ya maeneo (GPS) na kompyuta utatekelezwa kupitia Mradi wa Kuboresha Mtandao wa Maeneo ya Hifadhi Kusini mwa Tanzania (SPANEST) ili kuhakikisha kuwa kundi la wanyama jamii ya tembo wanalindwa na kuendelea kuishi ili vizazi vijavyo viione rasilimali hiyo muhimu.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Mratibu wa SPANEST, Godwell Olle Meingíataki kwenye ukumbi wa ofisi ya VETA Mkoa wa Iringa alisema kuwa, wako katika hatua za mwisho za utekelezaji wa mpango huo na kuongeza kuwa hatua ya kuwafunga tembo wote itakuwa imetafutiwa ufumbuzi mkubwa ambapo kila tembo atajulikana kwenye mtandao huo wa kompyuta.
"Kwa kupitia mpango huo tutakaoutekeleza ndani ya hifadhi zetu tembo, viongozi wa makundi ya tembo watafungwa kifaa maalumu shingoni kitakachokuwa kinatoa taarifa za mwenendo wao katika kila eneo watakalokuwepo ndani na nje ya hifadhi na tunahakika kupitia mpango huu tutawanusuru wanyama hawa," alisema Godwell.
Aliongeza kuwa, kwa kupitia kifaa hicho askari wa wanyamapori watakabiliana kirahisi na majangili wa meno ya tembo katika azma ile ile ya kunusuru kiumbe hicho kinacholiingizia Taifa mapato makubwa ya kigeni na kuwa kila kundi la tembo kwa sasa litakuwa linalindwa kwa umakini zaidi kwa kuwa litajulikana kiurahisi maeneo lilipo.
Alisema kuwa, kwa kupitia mradi wa SPANEST, Februari mwaka huu, Hifadhi ya Ruaha ilipata msaada wa vitendea kazi mbalimbali yakiwemo magari mawili ya doria yaliyotolewa na Shirika la Maendeleo ya Umoja wa Mataifa (UNDP) na kuongeza kuwa mpango huo wa kutoa msaada umewezesha zaidi kuimarika kwa ulinzi ndani ya hifadhi hiyo.
Alisema, vifaa vya mawasiliano vitafungwa katika magari hayo na mengine ya hifadhi hiyo ili kuwezesha mawasiliano na uchukuaji wa hatua za haraka pale zitakapotokea taarifa tata kuhusiana na tembo hao ambapo Oktoba hadi Novemba mwaka jana, Wizara ya Maliasili na Utalii ilifanya sensa ili kuiwezesha serikali kutambua hali ya rasilimali ya wanyamapori ndani na nje ya maeneo yaliyohifadhiwa.
Alisema kuwa, katika taarifa ya wizara hiyo inaonesha kwa kushirikiana na wataalamu wa ndani na nje ya nchi walifanya sensa katika maeneo ya mfumo wa ikolojia yenye tembo wengi ya Selous, Mikumi, Ruaha na Rungwa na kuwa matokeo hayo yanaonesha mfumo wa ikolojia wa Ruaha una tembo wengi kuliko hifadhi nyingine nchini ukiwa na tembo wapatao 20,090.
Matokeo hayo yanaonesha kwamba mfumo wa Ikolojia wa Selous-Mikumi kwa sasa una tembo wapatao 13,084 wakati mwaka 1976 kulikuwa na tembo 109,419 ambapo, Meingíataki alisema juhudi za makusudi zinazofanywa na serikali ikiwa ni pamoja na kuimarisha doria na operesheni maalum mbalimbali zitasaidia kupunguza wimbi la ujangili.

Chanzo:Majira

0 comments:

 
Powered by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Iringa Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa